BALOZI SEIF, SERIKALI YAKE INASUBIRI MAPENDEKEZO YA RASIMU YA SERA YA HABARI.

 Na Mwandishi Wetu, Zanzibar.

MAKAMU wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Iddi amesema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inasubiri kuyapokea mapendekezo yatakayowasilishwa ya  Rasimu ya Sera ya Habari Zanzibar ili kuyafanyia kazi ili aone Sekta ya Habari Nchini inakuwa  imara.

Aidha Taasisi zinazohusika  na jukumu la kusimamia masuala hayo ni vyema zikahakikisha kwamba zinaharakisha mapendekezo hayo ili ile dhana ya Uhuru wa kupata Habari bila ya kuogopa inapatikana.

Katika taarifa iliyotumwa kwenye vyombo vya habari  leo na Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Othman Khamis Ame, inasema leo , Balozi Seif Ali Iddi alitoa kauli hiyo wakati wa mazungumzo yake na Uongozi wa Baraza la Habari Tanzania (MCT)  ulioongozwa na Katibu  Mtendaji  Kajubi Mukajanga aliokutana nao Ofisini kwake Mtaa wa Vuga Mjini Zanzibar.

Alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeahidi kutoa kila aina ya msaada katika kuona Sekta hiyo muhimu kwa jamii inawajibika ipasavyo katika kuwapasha habari wananchi.

“Habari ni Sekta muhimu inayotoa Taarifa na Elimu na kuwahusisha moja kwa moja wananchi wa kawaida wakiwemo wakulima vijijini ”. alisema Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar.

Pia Balozi Seif kupitia Uongozi wa MCT aliwakumbusha wanahabari kuzingatia sheria na maadili ya kazi katika kuandika habari wanazozifanyia utafiti wa kina ili zisaidie wananchi kupata habari za ukweli.

Alisema changamoto ya Vitambulisho vya Kazi inayowakumba wana habari wanaotokea Tanzania Bara na kupangiwa kufanya kazi Zanzibar Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliahidi kulifuatilia kwa kina suala hilo ambalo bado halijawa kero kama yalivyo masuala mengine katika utendaji.

“Waandishi wa Habari wanaotokea Tanzania Bara wanapaswa kuandaliwa utaratibu maalum wa kupata vibali vya kazi kwa vile wao hawahusiani  na kuwa na  Vitambulisho vya Mzanzibari Mkaazi katika kuomba kibali cha kufanya Kazi Zanzibar,”alisema

Alieleza kuwa mfumo unaotumika katika kuwapasha habari wananchi wa pande zote za Muungano hauna mipaka  licha ya kwamba Sekta ya Habari sio Taasisi iliyomo ndani ya masuala ya Muungano.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  aliupongeza Uongozi ( MCT) kwa umakini wao wa kusimamia Sekta ya Habari Nchini.

Naye Katibu Mtendaji wa MCT,  Kajubi Mukajanga alisema Kamati ya Maadili ya baraza hilo  imekuwa  na utaratibu wa kufanya ziara za kusikiliza malalamiko yanayotolewa na  wananchi wanaoandikwa visivyostahiki katika vyombo mbali mbali vya Habari.

Alisema Wajumbe wa Kamati hiyo kupitia ziara hizo hupata fursa za kushauri, kuelekeza pamoja na kuwaonya na wengine kuwachukuliwa hatua za kisheria wana habari  wanaofanya makosa  katika kuandika habari chafu dhidi ya wananchi.

Naye Mkuu wa  MCT  upande wa Zanzibar, Shifaa Hassan,  alisema Mchakato wa Sera ya Habari Zanzibar  umeanza tokea mwaka 2010 kwa mashirikiano baina ya Idara ya Habari Maelezo, Tume ya Utangazaji Zanzibar pamoja na baadhi ya Viongozi wa Taasisi za Serikali.

Shifaa alisema Zanzibar imekuwa tajiri katika masuala ya Historia ya Habari kutokana na kuanza mapema kwa Sekta hiyo ndani ya Ukanda mzima wa Afrika ya Mashariki.

Alisema Ofisi ya Baraza la Habari Tanzania upande wa Zanzibar ilianzishwa mwaka 2003 na kuanza na Mpango Maalum  wa harakati za kutoa mafunzo kwa Wana Habari wachanga  wa vyombo mbali mbali vya Habari wakiwemo pia wale waliomaliza masomo yao ya sekondari walioamua kujiunga na Tasnia hiyo. 
  Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari Bwana Kajubi Mukajanga akimkabidhi Balozi Seif  Vitabu mbali mbali vilivyochapishwa na Baraza hilo kuhusu Tasnia ya Habari Tanzania.
Balozi Seif akiwa katika picha ya pamoja na Uongozi wa juu wa Baraza la Habari Tanzania mara baada ya kubadilishana mawazo Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar, Kushoto ya Balozi Seif ni Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari, Kajubi Mukajanga na Muandishi wa Makala wa MCT Yussuf  Mpinga.
 
 Katibu Mtendaji wa Baraza la Habari (MCT) Kajubi Mukajanga Kulia ya Balozi Seif akielezea mikakati ya Baraza la Habari Tanzania inavyofanya kazi Zanzibar katika kuhakikisha Maadili ya Habari yanazingatiwa na wanahabari wote Nchini.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akizungumza na Uongozi wa Baraza la Habari Tanzania MCT uliofika Ofisini kwake Vuga Mjini Zanzibar kubadilishana nao mawazo.

Comments

Popular posts from this blog

SERIKALI YAREJESHA KAMBI TANO ZA JKT ZILIZOKUWA ZIMESITISHA MAFUNZO YA JESHI.

BELENG’ANYI, MBUNIFU MWENYE MALENGO YA KUTENGENEZA MGODI WA KUFUA UMEME.