WAKULIMA WA ZAO LA VITUNGUU IRINGA WATELEKEZA MASHAMBA.

Na Mwandishi Wetu, Iringa

BAADHI ya wakulima wa zao la vitunguu wilayani Iringa wamelazimika kutelekeza na kuacha kuhudumia mashamba yao kutokana na kukosa masoko ya uhakika hali ambayo imewaathiri kiuchumi, kisaikolojia na kuuwa mitaji yao.

Wakizungumza na mwandishi wa blog hii, mashambani huko yaliyopo eneo la Kiwere wilayani Iringa wakulima hao ,walisema  pamoja na kuacha kuhudumia mashamba yao bado wanailalamikia serikali kuweka ushuru mkubwa wa kodi ya mazao kwenye mageti pamoja na wanunuzi kutaka wakulima hao wauze mazao yao kwa lumbesa.

 Idhaa Ally alisema  kutokana na changamoto hizo wakulima wengi wameathirika kiuchumi na kisaikolojia kutokana na wengi wao kukopa fedha benki kwa ajili ya kilimo.

“Sisi tunatumia gharama kubwa kuanzia kuandaa shamba hadi kuvuna lakini changamoto inakuja kwenye soko na ukiangalia wengi wetu wakulima tumechukua mikopo na tunashindwa kurudisha kutokana na mazao kutonunulika.”alisema Ally.
Naye, Chacha Omary alisema  pembejeo za kilimo zimekuwa gharama kubwa sana  kiasi cha wakulima wadogo kushindwa kumudu gharama hizo.

Hata hivyo Omary aliiomba serikali kupunguza gharama za pembejeo za kilimo ili wakulima wadogo waweze kumudu gharama za pemebejeo hizo.
Elizabeth Chilala ambaye amelima hekari mbili alisema  ametumia zaidi ya Sh. Mil.4.5 lakini ameambulia kupata magunia 70  tu hali ambayo imemkatisha tamaa ya kuendelea kulima zao hilo kutokana na gharama za uendeshaji kuwa kubwa.

Chilala alisema  matarajio yake alikuwa auze gunia moja kwa sh.100,000 hadi 150,000 lakini hali imekuwa tofauti na kulazimika kuuza kwa gunia moja kwa sh. 50,000.
 Ofisa Kilimo wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa, Lucy Nyalu alikiri changamoto hiyo na kusema wao kama serikali wanawahamasisha wakulima kulima kilimo cha kibiashara ili kujihakikishia kuwa na kipato pamoja na chakula cha uhakika.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Iringa Vijijini, Robert Masunya, alisema  Halmashauri inatambua masuala ya lumbesa na pia inatambua  sheria ya wakala wa vipimo ya mwaka 2002 sura ya 340 ambayo inatoa mwelekeo mzima juu ya usimamizi wa mazao kwa kuzingatia uzito.

PICHA KWA MSAADA WA MTANDAO

Comments

Popular posts from this blog

SERIKALI YAREJESHA KAMBI TANO ZA JKT ZILIZOKUWA ZIMESITISHA MAFUNZO YA JESHI.

BELENG’ANYI, MBUNIFU MWENYE MALENGO YA KUTENGENEZA MGODI WA KUFUA UMEME.