BELENG’ANYI, MBUNIFU MWENYE MALENGO YA KUTENGENEZA MGODI WA KUFUA UMEME.


Peter Akaro

BINADAMU anazaliwa na ubunifu au mazingira anayokuliwa yanaweza kumfanya kuwa hivyo.

Makala ya leo yatazungumzia maisha ya mbunifu Ntibanga Beleng’anyi ambaye anatengeneza mashine za kukamulia juisi ya miwa na kuunda magari.

Pengine vitu hivi si vigeni katika mazingira yetu, ila kilichopelekea makala haya kuandikwa, ni namna Beleng’anyi alivyoweza kutengeneza vitu hivi bila kusomea sehemu yoyote.

Ndiyo hakusoma, Baada ya kumaliza Shule ya Msingi Ng’wang’iwita iliyopo Bariadi Shinyanga, mwaka 2005 aliamua kuja Dar es Salaam kwa ajili ya kazi za kibunifu kwa sababu upatinaji wa vifaa ni rahisi, vitu alivyofanikiwa kutengeneza ni kama.
Hii ni mashine ya kutengenezea juisi ambayo inatembea umbali wa kilo mita 400.

MASHINE YA JUISI.

Mashine ya kukamua juisi ya miwa ambayo kaitengeneza yeye ina utofauti katika vitu viwili ukilinganisha ni zile zilizozoeleka, kwanza mtumiaji ana uwezo wa kuitembeza hadi umbali wa meta 400 kutokana ina matairi.

Pili mashine inapokuwa inafanya kazi inaweza kuzalisha umeme wake kwa ajili taa na hata redio, hapa ni pale injini inapokuwa inafanya kazi na hata itakapozimwa umeme uliozalishwa unahifadhiwa.

Pia matumizi yake ya mafuta si makubwa sana, kwani lita mbili zinaweza kutumia ndani ya masaa sita ila inatengemea na matumizi ya muhusika.

“Tokea mwaka jana ninatengeneza hizi mashine, gharama zinatofautiana kulingana na upatikanaji wa vifaa, kwa hiyo bei inaweza kuwa kati ya sh. milioni mbili hadi tatu,” anasema.

Anaeleza kuwa alianza kazi ya kutengeneza hizi mashine kutoka na kupenda kuwa mjasiriamali katika ufundi stadi ili kuweza kujikwamua kimaisha.

“Unapoona kazi inatendeka kwa kiasi fulani inabidi mbunifu uindeleze zaidi ili kuleta matokeo bora zaidi,” anasema Beleng’anyi.

KUUNDA MAGARI.

 “Niliamua kuanza kuunda magari kwa sababu hakuna sehemu ya kwenda kuajiriwa na pia sijapita katika mfumo wa kuweza kutambulika,” anasema
Gari alilounda mwaka 2012 lilikuwa linatumia mafuta lita moja kwa kwenda umbali wa kilometa 18 hadi 20, na lilikuwa linaenda kwa spidi 50 hadi 80 kwa saa moja ila ilitengemea na aina ya barabara pia.


“Niliachana na mpango wa kuunda magari kutokana na kusumbuliwa barabarani na polisi, waliniuliza kwa nini umetengeneza kitu ambacho hakina usajili wala kadi, pili walikuwa wakisema huu ni mtambo na si gari, nilipoona usumbufu umezidi ndipo nikalipeleka kijijini kwetu.

“Zilikuwa ni ndoto zangu tangu nikiwa nasoma nilisema siku moja nitaunda gari, kama ningepata shule ya moja kwa moja ningekuwa mbali sana, na hivi vyote ninavofanya sasa si kwamba vimeibuka tu kipindi hiki bali ni ndoto za muda mrefu,” anasema na kuongeza.

“Nilijaribu kwenda kufanya usajili wa gari wakanieleza nipeleke nyaraka zitazoonyesha gari limenunuliwa nchi gani, limetembea umbali gani, niliposhindwa hayo nikalipelekea kijijini kama nilivyoeleza awali,” anasema.
Anaeleza kwa sasa gari kijijini linatumika kwa kubeba maji na mizigo mbali mbali yenye uzito wa hadi kufikia tani moja.

“Gari hili linafaa kwa matumizi ya kijijini kwa sababu licha ya kukusafirisha, linaweza kuvuta maji kwenye kisima, na pia ukafunga kinu kwa ajili kukoboa mahindi au mpunga,” anasema.
  Hili ni gari ambalo aliliunda ila  kutokana na usumbufu aliokuwa akiupata barabarani aliamua kurudisha kijijini.


WALIOSOMEA FANI WANAFANYA NINI.

Pengine waliopita katika mfumo rasimi, yaani shule muda mwingine wanaweza wasiweze kufanya kama yeye, je nini kinapelekea hali hiyo?
Anajibu kwa kusema wengi (wanafunzi) wanakwama kwa sababu wanachofundishwa mara nyingi ni tofauti na kile ambacho wanatakiwa wakifanye kwa vitendo.

“Kuna vitu vinakuwa vinakinzana, siku zote ubunifu huwa ni wa mtu, hakuna shule ambayo utafundishwa hilo au kufikiria, shule unafundishwa tu zile kanuni za msingi, lakini katika muendelezo wa maisha hautakiwi kukariri bali kuwa mbunifu,” anasema Beleng’anyi.

Anaeleza kuwa licha ya wabunifu wengi kuonyesha uwezo mkubwa hakuna jitihada za makusudi zinazofanyika ili kuwainua.

“Hata nilipotengeneza lile gari nilienda Tume ya Sayansi na Teknolojia (Costech) wakaniambia sawa umetengeneza gari, lakini umetumia vifaa vya watu wengine inabidi ni tengeneze vyangu.

“Hii dunia ina kila kitu, kinachotakiwa ni wewe kuvikusanya na kuunda unachotaka, sasa ukianza kila kitu utengeneza wewe utakuwa ndio umeanza mwanzo, na gharama zitakuwa kubwa,” anasema.

 MALENGO YA BAADAYE.

Beleng’anyi anasema malengo yake si kuendelea kutengeneza vitu vidogo vidogo kama hivi, bali ni kutengeneza ‘mgodi’ wa kufua umeme na tayari ameshafanya utafiti na kugundua anaweza kuzalisha kwanzia KV 30 hadi Megawatts 10 za umeme.

“Sasa hivi serikali imekuwa na mkakati wa kupeleka umeme vijijini, ila mimi nitakuja na mkakati wa kupeleka umeme mashambani.

“Ina maana tuchimbe visima kwa ajili ya umwagiliaji na ufugaji, hii itakuwa na faidi kuliko kupeleka umeme kijijini kwa ajili ya kuwasha taa tu, hiyo haiwezi kumletea mwananchi maendeleo bila kuwa na shughuli za kiuzalishaji,” anasema na kuongeza.

“Itawezekana kwa sababu tupo katika mabadiliko ya ukuaji wa viwanda, tunatakiwa tushindane katika hoja za kitenolojia na si vingonevyo, cha msingi serikali ituangalie,” anasema Beleng’anyi.








Comments

Popular posts from this blog

SERIKALI YAREJESHA KAMBI TANO ZA JKT ZILIZOKUWA ZIMESITISHA MAFUNZO YA JESHI.