MFUMUKO WA BEI WA TAIFA KWA MWEZI JUNI, 2017 UMEPUNGUA.

 Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii wa Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Ephraim Kwesigabo (kushoto) akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam wakati wa kutangaza Mfumuko wa Bei wa Taifa wa mwezi Juni, 2017 ambao umepungua hadi asilimia 5.4 kutoka asilimia 6.1 mwezi Mei, 2017. Kushoto kwake ni Meneja wa Takwimu za Bei na Ajira, Ruth Minja.

Baadhi ya Waandishi wa habari waliohudhuria katika Mkutano wa kutangaza Mfumuko wa Bei wa Taifa wa mwezi Juni, 2017 uliofanyika jana jijini Dar es Salaam. Mfumuko wa bei umeonyesha kupungua hadi asilimia 5.4 kutoka asilimia 6.1 mwezi Mei, 2017.

 ( PICHA NA EMMANUEL GHULA)

Na,Veronica Kazimoto.

MFUMUKO wa Bei wa Taifa kwa mwezi Juni, 2017 umepungua hadi asilimia 5.4 ikilinganishwa na asilimia 6.1 ilivyokuwa mwezi Mei, 2017.

Akizungumza na waandishi wa Habari jana jijini Dar es salaam, Mkurugenzi wa Sensa ya Watu na Takwimu za Jamii kutoka Ofisi ya Taifa ya Takwimu, Ephraim Kwesigabo amesema Mfumuko wa Bei umepungua kutokana na kupungua kwa kasi ya mabadiliko ya bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Juni, 2017 ikilinganishwa na kasi ya upandaji iliyokuwa kwa mwezi Mei, 2017.

“Mfumuko wa Bei wa mwezi Juni, 2017 umepungua hadi kufikia asilimia 5.4 kutoka asilimia 6.1 mwezi Mei, 2017. Hii inatokana na kupungua kwa kasi ya upandaji wa bei za bidhaa na huduma kwa mwezi Juni, 2017,” amesema Kwesigabo.

Amesema Mfumuko wa Bei unaopimwa kwa kipimo cha mwezi umepungua kwa asilimia 0.1 ikilinganishwa na ongezeko la asilimia 0.2 ilivyokuwa mwezi Mei, 2017.

Kwesigabo amesema Fahirisi za Bei zimepungua hadi 109.10 mwezi Juni, 2017 kutoka 109.26 mwezi Mei, 2017. Amesema Kupungua kwa Fahirisi za Bei kumechangiwa hasa na kupungua kwa bei za baadhi ya bidhaa za vyakula.

Baadhi ya bidhaa za vyakula zilizochangia kupungua kwa fahirisi ni pamoja na mahindi ambayo yamepungua kwa asilimia 5.1, unga wa mahindi kwa asilimia 2.4, unga wa mihongo kwa asilimia 1.9, machungwa kwa asilimia 2.4, dagaa kwa asilimia 3.2, mbogamboga kwa asilimia 5.7, maharage kwa asilimia 1.8 na viazi mviringo kwa asilimia 6.2.

Aidha Mfumuko wa Bei kwa bidhaa za vyakula nyumbani na migahawani kwa mwezi Juni, 2017 umepungua hadi asilimia 9.8 kutoka asilimia 11.8 mwezi Mei, 2017.

Uwezo wa Shilingi 100 ya Tanzania katika kununua bidhaa na huduma umeimarika kidogo na kufikia Shilingi 91 na senti 66 mwezi Juni, 2017 ikilinganishwa na Shilingi 91 na senti 53 ilivyokuwa mwezi Mei, 2017.

Hata hivyo, Mfumuko wa Bei nchini Tanzania una mwelekeo unaofanana na baadhi ya nchi nyingine za Afrika Mashariki kwa kuwa Mfumuko wa Bei wa mwezi Juni, 2017 nchini Uganda umepungua hadi asilimia 6.4 kutoka asilimia 7.2 mwezi Mei, 2017; na nchini Kenya, Mfumuko wa Bei wa Mwezi Juni, 2017 umepungua hadi asilimia 9.21 kutoka asilimia 11.70 mwezi Mei, 2017.

Comments

Popular posts from this blog

SERIKALI YAREJESHA KAMBI TANO ZA JKT ZILIZOKUWA ZIMESITISHA MAFUNZO YA JESHI.

BELENG’ANYI, MBUNIFU MWENYE MALENGO YA KUTENGENEZA MGODI WA KUFUA UMEME.