ASKOFU MWAMAKULA AIOMBA SERIKALI KUWACHUKULIA HATUA WANAOTUMIA DINI KUWARUBUNI WATU.



Na Enles Mbegalo

ASKOFU  Mkuu wa Dayosisi Kuu ya Dar es Salaam na Mkuu wa Kanisa la Moravian la Uamsho Tanzania (KMUT), Emmaus Mwamakula, amemuomba Rais John Pombe Magufuli, kupitia Taasisi na vyombo vyake kuwachunguza na kuwachukulia hatua watu wote wanaotumia dini katika kuwarubuni watu.

Akizungumza na mwandishi wa blog hii leo, jijini Dar es Salaam, Mwamakula alisema afya za watu zitakuwa salama endapo serikali itazuia uholela katika uendeshaji wa vikundi vya dini kwa kuhakikisha  viongozi wa dini wanakuwa na mafunzo, maadili na historia inayoeleweka.

Askofu Mwamakula alitoa wito kwa watu wanaotapeliwa na watu wanaotumia kivuli cha dini kuanza kujitokeza hadharani kwa kutoa taarifa katika vyombo vya sheria  ili  kuweza kuzuia machafuko katika nchi kwa kutunza afya za watu.

“Ninaiomba serikali yetu kuhakikisha kuwa watu wanaoongoza Taasisi za Dini wawe ni  watu ambao historia zao zinajulikana hasa kuhusiana na wapi watu hao walipata mafunzo yanayohusiana na shughuli zao,”

Alisema ifike mahali jamii ielewe kuwa mambo ya imani yakiachwa yaendeshwe kiholela na watu  ambao hawana mafunzo na uongozi thabiti itakuwa hatari kubwa.

“Nchi  inapokuwa na watu wenye afya nzuri katika mambo haya matatu  uchumi, usalama na ustawi wake unakuwa ni wa uhakika kwani katika miaka ya hivi karibuni jamii yetu imeshuhudia watu ambao historia ya  mafunzo yao hayajulikani lakini wamekuwa wakianzisha Taasisi za Dini huku uendeshaji wake ukiwa mikononi mwa watu binafsi,”alisema Askofu Mwamakula na kuongeza

“ Ustawi wa jamii yeyote ile duniani unategemea sana afya ya kiakili, kimwili na kiroho kwa wanajamii husika na imani potofu zinaweza kuathiri uchumi, usalama na ustawi wa jamii,”

Pia Askofu Mwamakula alitoa mfano wa kuibuka kwa wingi wa vikundi vya dini ambavyo viongozi wao hutoa ahadi za kuwaponya watu watakaotoa fedha vitendo  ambavyo  hupelekea kuwafilisi wahanga.

Comments

Popular posts from this blog

SERIKALI YAREJESHA KAMBI TANO ZA JKT ZILIZOKUWA ZIMESITISHA MAFUNZO YA JESHI.

BELENG’ANYI, MBUNIFU MWENYE MALENGO YA KUTENGENEZA MGODI WA KUFUA UMEME.